SOMA MAKALA HII UONE JINSI SHIVJI ALIVYOPONDA MCHAKATO WA KATIBA MPYA


MWANASHERIA NGULI PROFESA ISSA SHIVJI


Asema umehodhiwa na wanasiasa na kutahadharisha usipoangaliwa unaweza kuzaa machafuko.
Dodoma.  Mwanazuoni na  Mwanasheria nguli, Profesa Issa Shivji  ameuponda mchakato wa Katiba Mpya kuwa umehodhiwa na wanasiasa na kutahadharisha kuwa usipoangaliwa vizuri unaweza kusababisha machafuko.
Aliyasema hayo jana mjini hapa alipokuwa akitoa mhadhara kwa Jumuiya ya Chuo Kikuu cha Dodoma, (Udom). Mhadhara huo uliandaliwa kama sehemu ya mafunzo kwa ajili ya wanafunzi wanaojiandaa kuhitimu masomo yao (Convocation ).
Profesa Shiviji ambaye alitumia saa 1.15 kutoa mhadhara wake juu ya mchakato wa Katiba, alisema Bunge la Katiba lipo juu ya Bunge la Kawaida.
Alisema katika historia ya Tanzania imewahi kuwa na mabunge mawili yaliyoandaliwa kupata Katiba, lakini yote hayakuwa na wabunge waliochaguliwa.
“Tukiangalia katika historia hatukuwahi kuwa na Bunge la Katiba ambalo lilichaguliwa na wananchi. Safari hii tulikuwa na nafasi ya kuwa na Bunge ambalo lilichaguliwa na wananchi lakini kwa bahati mbaya hakuna nafasi ya kufanya hivyo ,”alisema.
Kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, wabunge wote 357 na Wawakilishi 81 watakuwa ni wabunge wa Bunge Maalumu la Katiba huku mashirika yasiyo ya kiserikali yakipewa wawakilishi 20.
Wajumbe wengine ni vyama vya siasa vyenye usajili wa kudumu 42, wawakilishi wa taasisi za elimu ya Juu 20, watu wenye mahitaji maalumu (20), vyama vya wafanyakazi (20), wafugaji (10), wavuvi (10), wakulima (20) na makundi mengine yenye mahitaji muhimu ni wawakilishi (20).
Profesa  Shivji  alisema Bunge la Katiba litakuwa na jumla ya wabunge  639, ambapo 438 asilimia 69  ya wabunge wa Bunge hilo wanatokana na vyama vya siasa.
Alisema kati ya wabunge hao kutoka vyama vya siasa asilimia  52 ni Wana-CCM na asilimia 16  ni kutoka vyama vya upinzani.
“Katika wajumbe 42 watatokana na vyama vya kisiasa, kwa hivi itafanya jumla ya wabunge la Katiba ambao watatokana na vyama vya siasa kuwa ni asilimia 75;
“Kama hesabu zangu ni sahihi ama zinakaribia wabunge wanaotokana na CCM watakuwa ni  asilimia 63, wapinzani asilimia 27 na wasiokuwa na chama ni asilimia 10,”alisema.
Alisema kwa kuangalia idadi ya wajumbe wanaotokana na mashirika yasiyo ya kiserikali wana uwiano sawa na wawakilishi wa mashirika ya wavuja jasho yaani wakulima, wavuvi, wafugaji na wanazuoni.
Alihoji mashirika yasiyo ya kiserikali yanawawakilisha kina nani katika Bunge hilo na mashirika hayo bila ya aibu yamejigeuza kuwawakilisha wananchi wakati hiyo siyo sahihi kwa kuwa hawahusiki na wananchi moja kwa moja.
“NGO’s zina nafasi ya wawakishi sawa, lakini si wawakilishi wa wananchi hawakuchaguliwa na wananchi, wala hawawajibiki kwa wananchi hali halisi wanawajibika zaidi kwa wafadhili, katika sheria  hii NGOs ndio wamepewa kipaumbele kana kwamba ni sawa na wananchi,” alisema Shivji na kushangiliwa.
Kwa upande wa kura ya maoni, Profesa Shivji alikikosoa kipengele katika sheria ya kura ya maoni ambayo inatarajiwa kuletwa Bungeni katika mkutano wa 14 wa Bunge.
Alisema katika sheria hiyo inataka ili jambo likubaliwe ni lazima lipate kura za ndiyo asilimia 50 kwa kila upande muungano.
Alisema hilo litafanya watu wachache waamue kwa ajili ya walio wengi.
Alifafanua kuwa kwa mujibu wa sheria hiyo asilimia 50 inayotakiwa ni ya kura halali na wala si inayotokana na idadi ya wapiga kura waliopo kisheria katika Bunge hilo.
Aidha, Profesa Shivji aliwataka wasomi wanapoona mambo yanaharibika kusema badala ya kusubiria mambo yaharibike ndipo waseme.
Alisema mchakato mrefu katika kupata Katiba ni muhimu sana na hautakiwi kuharakishwa.
“Jambo hili linatakiwa kuwa na muda wa kutosha badala ya kuweka ratiba ya miezi, miaka, unatoa mwanya kwa matapeli wa kisiasa kupenyeza na wanaweza kuleta vurugu kubwa sana,”alisema.
Alisema suala la kuwapa wataalamu kuandika Katiba bila ya kuwa na sheria ni kuwapa nafasi wanasiasa kuuvuruga.
Share this post :

Chapisha Maoni


Get This:Techkgp

PAGE VIEWERS

About Me

Blog Archive

Blog za rafiki zangu

Get This:Techkgp
3D Live Statistics
 
Support : The Bantu | Mufandish | Mufandish Inc
Copyright © 2011. MUFANDISH NEWS - All Rights Reserved
Template Created by Mufandish Inc Published by Mufandish Mufandish
Proudly powered by Blogger